Tuesday, January 8, 2013

UTEKELEZAJI WA ILANI YA UCHAGUZI 2005-2012-SINGIDA


Na Boniface Mpagape.

Taarifa ya utekelezaji wa ilani ya uchaguzi ya tangu mwaka 2005 hadi mwaka 2012, imedhihirisha kuwa mkoa wa Singida umepiga hatua kubwa katika kutekeleza miradi ya maendeleo katika kipindi hicho.

Akitoa taarifa ya utekelezaji wa ilani hiyo jana kwa waandishi wa habari, wakuu wa wilaya za mkoa huo, na wataalam wa sekretarieti ya mkoa, Mkuu wa mkoa huo Dr. Parseko Ole Kone  amebainisha kuwa malengo mbalimbali yamefikiwa.

Katika sekta ya utawala bora, ameeleza kuwa mwaka 2005 mkoa ulikuwa na majimbo matano ya uchaguzi na mwaka 2012 kuna jumla ya majimbo manane ya uchaguzi.

Aidha wilaya mpya mbili zimeanzishwa na kufanyamkoa wa Singida kuwa na jumla ya wilaya tano. Kata zilikuwa themanini na nane na sasa zipo mia moja ishirini na nne. Kulikuwa na vijiji mia tatu sitini na sita na sasa vipo mia nne arobaini na mbili.

Kuhusu sekta ya kilimo katika kipindi hicho mkoa uliweka kipaumbele katika mazao ya chakula  kama mtama, uwele, viazi vitamu, muhogo na maharage mazao ambayo huvumilia ukame.  Mkuu huyo wa mkoa ametaja mazao ya biashara yanayolimwa mkoani  humo ni alizeti, vitunguu, ufuta, pamba pamoja na zao la porini la asali. Taarifa hiyo imeonyesha kuna mafanikio makubwa kutokana na ongezeko la uzalishaji toka mwaka 2005 hadi 2012.

Aidha Bw. Kone amesema mkoani Singida kuna ongezeko kubwa la viwanda kutoka viwanda hamsini hadi kufikia tisini, sambamba na idadi ya wafanyabiashara kuongezeka.  Katika kipindi hicho pia sekta ya elimu imeonyesha mafanikio makubwa kwani shule za awali, msingi, sekondari pamoja na vyuo, imeongezeka.

Taarifa hiyo imetaja sekta ya afya kuwa imeonyesha mafanikio kutokana na ongezeko la zahanati, vituo vya afya na kwamba hospitali mpya ya mkoa inajengwa eneo la Mandewa na baadhi ya majengo yamekamilika.  Amesema mafanikio katika chanjo kwa watoto yametokana na idadi ya watoto waliochanjwa kuongezeka na kuufanya mkoa wa Singida kuwa wa pili kitaifa. 

Mkuu huyo wa mkoa wa Singida amesema vifo vya watoto wenye umri wa chini ya miaka mitano imepungua kutokana na kusogezwa kwa huduma za afya kwa wananchi.  Amesema vifo vitapungua zaidi kutokana na kuanzishwa kwa chanjo mpya ya magonjwa yanayosumbua watoto iliyozinduliwa mwishoni mwa mwaka uliopita.

Kuhusu  mapambano dhidi ya ugonjwa wa UKIMWI, miongoni mwa watu elfu tano mia tisa na thelethini na tatu waliopima mwaka 2005, waliokuwa na maambukizi ni watu mia tatu na tatu.  Amesema mwaka 2012 jumla ya watu elfu ishirini na tatu na sabini na wawili walipima na mia nane tisini na tisa walikuwa wamepata maambukizi ya virusi vya ukimwi, sawa na asilimia tatu nukta tisa hali ambayo inaonyesha pia kuwa kiwango cha  maambukizi kinashuka.

Taarifa hiyo imesema kuwa katika sekta ya barabara kwa kiwango cha lami, mkoa wa Singida mwaka 2005 ulikuwa na kilomita moja tu ya lami na sasa zaidi ya kilomita mia tatu sitini na nane, zimejengwa kwa kiwango cha lami. 

Kutokana na mkoa wa Singida kukabiliwa na tatizo la uhaba wa maji kwa muda mrefu, mkoa umeongeza idadi ya vyanzo vya maji na kwamba mradi mkubwa wa maji unatekelezwa chini ya udhamini wa Benki ya kiarabu kwa kushirikiana na serikali. Amesema mradi huo unagharimu dola za kimarekani milioni kumi na tisa. 

Mkuu wa mkoa wa Singida Bw. Parseko Kone amesema mradi huo utakapokamilika,  jumla ya mita za ujazo ishirini na moja elfu zitazalishwa kwa siku ambazo amesema zitatosheleza mahitaji ya maji kwa wakazi wa Singida hadi mwaka 2025.

 

 

No comments: