Monday, July 29, 2013

MADIWANI 16 WA CHADEMA WASUSIA MKUTANO HANANG


Na:Mwandishi wetu
Madiwani 16 wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) wa halmashauri ya wilaya ya Hanang, mkoani Manyara juzi walisusia mkutano wa Baraza la Madiwani wa Halmashauri hiyo na kuamua kutoka nje ya ukumbi wakidai kanuni za mkutano huo zimekiukwa.

Akizungumza na Waandishi wa habari nje ya ukumbi wa mkutano huo, Mbunge wa viti maalum Mkoa wa Manyara kupitia tiketi ya CHADEMA, Bi.  Rose Kamili amesema madiwani hao waligoma kujiandikisha kwenye orodha ya wajumbe baada ya kutokubaliana na dondoo zilizokuwepo kwenye mkutano huo, ikiwemo ya uchaguzi wa makamu mwenyekiti wa Halmashauri hiyo na kupitisha kamati za kudumu.

Aidha mbunge huyo amesisitiza pia kwamba licha ya madiwani wa chama hicho kudai mabadiliko ya maamuzi hayo kabla ya kusoma muhtasari wa kikao, mwenyekiti alitumia ubabe kulazimisha kikao hicho kuendela na kwamba hakuwa tayari kusikiliza wazo la mtu ambaye hajajiandikisha kwenye mahudhurio ya mkutano huo.

Akihalalisha kufanyika kwa mkutano huo, Mwanasheria wa TAMISEMI,Bw. Eustad Atanas Ngatale amesisitiza kuwa taratibu za mikutano ya halmashauri zinaongozwa na kanuni za uendeshaji wa mikutano ya halmashauri ambazo zinatungwa na halmashauri yenyewe lakini uwezo huo umetolewa na Waziri mwenye dhamana ya serikali za mitaa.

No comments: