Thursday, August 9, 2012

TANZANIA KUITWANGA MALAWI KAMA IDDI AMINI?

Mhe. Lowasa (waziri mkuu mstaafu) Kitoa msimamo wa kamati ya Bunge kuhusu dalili na vitisho vya MALAWI kutaka kuliteka ziwa Nyasa, hii ni dalili ya yaliyotokea miaka ya sabini wakati IDIAMINI DADA wa Uganda alipojaribu kuuteka mkoa wa Kagera kwa madai kuwa ni mali yake, Pamoja na vifo na jasho jingi Tanzania iliukomboa na hatimaye kumong'ao Idiamini nchini Uganda na akakimbilia kwa Muamar Ghadaffi nchini LIbya hadi alipokutwa na MAUTI
endelea................

KAMATI ya Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama imesema Tanzania imejiandaa kiakili na kivifaa kuingia vitani na Malawi kama italazimika kufanya hivyo.Akizungumza mjini Dodoma jana, Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Edward Lowassa alisema kamati yake imeridhishwa na maandalizi ya Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ).

“Tumepewa maelezo na jeshi letu na tumeridhika kuwa ikibidi kuingia vitani jeshi letu liko vizuri sana na limejipanga vizuri sana kwa uhakika, kiakili na kivifaa,” alisema Lowassa.

Kabla ya Lowassa kuzungumza na waandishi wa habari, alifanya kikao cha faragha kilichohusisha pia wajumbe wa kamati hiyo na makamanda wa JWTZ walipofika bungeni kutoa taarifa kwa kamati hiyo.
Hata hivyo, katika tamko hilo Lowassa alisema Tanzania inatarajia mgogoro huo utamalizika kwa njia za kidiplomasia kwa sababu Watanzania na Wamalawi ni ndugu wa muda mrefu.

“Ikibidi kuingia vitani jeshi letu liko vizuri sana na kama ilivyo ahadi yao (JWTZ), wako tayari kulinda mipaka ya nchi yetu hadi tone la mwisho. Tunasali sana tusifike hapo,” alisema Lowassa na kuongeza: “Tunategemea hatutafika huko, lakini kwa heshima ya nchi yetu kama ikibidi kufika huko (vitani) tutafika kulinda mipaka yetu”.

Mwenyekiti huyo ambaye aliwahi kuwa Waziri Mkuu, alisema kama Tanzania itafikishwa mahali itabidi damu ya Watanzania imwagike, nchi iko tayari kulinda mipaka yake kwa nguvu.Alisema kama itabidi kuingia vitani, itatumia umoja na mshikamano wa Watanzania wa mwaka 1978 wakati wa Vita na Uganda kulinda mipaka ili kulinda heshima ya nchi.

Alisema mwaka 1978 wakati Rais wa Uganda, Idd Amin na majeshi yake walipochukua sehemu ya Tanzania na kujitangazia ni mali yake, ilichukua hatua kumfukuza Amin.

“Alijitangazia sehemu ile ni mali ya Uganda hutegemei nchi ikae kimya, hutegemei Watanzania wanyamaze wakati nchi yao imetekwa, tulichukua hatua tukamfukuza hadi nchini kwake.”
Lowassa alisema Kamati ya Bunge inajua madhara ya kiuchumi yaliyotokana na Vita ya Idd Amin na kwamba vita yoyote ikipiganwa lazima kunakuwa na madhara ya kiuchumi.

Hata hivyo, alisema anaamini mgogoro huo hautafika huko na kusisitiza kuwa, lakini ikibidi JWTZ ni moja kati ya majeshi bora duniani na ni jeshi lililojiandaa vizuri kwa lolote.
“Wako tayari sisi ni moja kati ya jeshi lililojiandaa vizuri na jeshi bora duniani na la kujivunia. Tuko imara kiakili na kivifaa tena vya kisasa,” alisema Lowassa.

Alisema kamati yake inaunga mkono msimamo ulitolewa bungeni juzi na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Bernard Membe kuhusu mgogoro huo na kwamba ndiyo kauli rasmi ya Serikali.
Juzi, Waziri Membe alizionya kampuni za kigeni za Malawi zilizoingia katika ardhi ya Tanzania eneo la Ziwa Nyasa kutafiti mafuta na gesi kusitisha mara moja.

Akiwasilisha makadirio ya wizara yake, Membe alisema upo ushahidi kuwa ndege tano za utafiti za Malawi ziliruka anga la Tanzania na kutua katika Ziwa Nyasa upande wa Tanzania.Membe alisema pamoja JWTZ kutoruhusu ndege hizo za Malawi kuingia na kutua eneo hilo la Ziwa Nyasa, bado ziliingia na kutua kinyume kabisa cha sheria za kimataifa.

“Wenzetu wa Malawi wanadai Ziwa Nyasa lote lipo Malawi na msingi wa madai yao ni mkataba wa Heligoland wa mwaka 1890 na sisi tunasema mpaka uko katikati ya Ziwa.”

Membe alisema hata mgogoro wa mpaka kati ya Cameroon na Nigeria ulitatuliwa na Mahakama Kuu ya Dunia kuwa mpaka baina ya nchi hizo mbili upite katikati ya Ziwa Chad.

Juzi, Waziri wa Mambo ya Nje wa Malawi, Patrick Kabambe alikaririwa na Redio Sauti ya Ujerumani akisema wataendelea na utafutaji mafuta licha ya onyo hilo la Tanzania.

Waziri huyo alisema ziwa hilo linaitwa Malawi na siyo Ziwa Nyasa na kwamba utafutaji wa mafuta na gesi utaendelea na hakuna wa kuwasimamisha. Alihoji, iweje Tanzania ishtuke sasa?

CHANZO: MWANANCHI COMMUNICATION

No comments: