Tuesday, October 9, 2012

VITUKO VYA WASOMI NA MITINDO YA MAVAZI VYUONI





Na Boniface Mpagape.
Kwa  mtizamo wangu mtu yeyote aliyepata fursa ya kupata elimu  anatakiwa kuwa mfano mzuri wa kuigwa na wale wengine wengi ambao hawakupata fursa hiyo na kuwa na uwezo mkubwa wa kuchambua mema na mabaya,  mazuri kuyaenzi  na machafu kuyatia kapuni.  



PICHA: Centre ya mtaa wa Ginnery, hapa ukipaona mchana huwezi kuamini endapo utapalinganisha na usiku tena iwe usiku wa Ijumaa na Jumamosi, salaaaaaleeeeeeeeeeeeeee, Mama yangu, wadogo zetu wakiwa mtaa huu Ijumaa ni BIKINI na Vichupi nje nje, kinachouma wengine wazazi wao wamekwama kulipa ada, wengine wamelipa baada ya kuteketeza mali za familia ikiwemo mashamba, sasa dada zetu wako vyuoni wakiiga kutembea uchi.

Kumbe  najidanganya!  Si mimi peke yangu bali hata wewe msomaji waweza kuniunga mkono haya

ninayosema, nadhani umeshawahi kusikia watu wakihoji elimu aliyoipata fulani inamsaidia nini?  Wengi hulinganisha matendo anayofanya msomi na kuyatafakari kwa kina hadi kufikia hitimisho la kuhukumu kwamba pengine kuelimika si suluhisho la kuwa kioo cha jamii ili hata wengine ambao hawakupata fursa ya kupata elimu waweze kuiga toka kwa msomi.

Mambo mengi mazuri yenye mtizamo wa kimaendeleo au kubadili hali ya maisha yetu kutoka katika umaskini uliokithiri na kutupeleka angalau katika kuyamudu maisha kwa kupata yale mahitaji muhimu katika maisha, yaani chakula, malazi na mavazi (yanayokubalika katika utamaduni wetu) yanapaswa kuigwa.

Kama kweli tungekuwa tunaiga labda fulani kajenga nyumba ya kisasa, lazima nami nijitahidi ingawa sina uwezo wa kujenga kama yake, lakini nijenge walau vyumba viwili na sebule.  Familia ya jirani yangu watoto wake wanapata lishe bora na hawasumbuliwi na utapiamlo nami wanangu nijitahidi kufanya kazi kwa bidii ili washibe wasipate utapiamlo, nadhani tungekuwa tumepunguza makali ya adui zetu watatu ambao ni ujinga, maradhi na umaskini, ambao bado naamini wamekita mizizi yao mirefu katika jamii yetu.
Hadi kufikia uamuzi wa kuyaandika haya, nimefanya utafiti kuhusu suala ambalo nimeliweka katika mabano hapo juu, lakini si vibaya endapo nikikukumbusha. Ni kuhusu mavazi yanayokubalika katika utamaduni wetu. 
Kwa kipindi kifupi ambacho nimefika Singida mjini nimeona mengi sana kuhusu suala hilo, hasa kwa dada zetu ambao napishana nao barabarani usiku lakini walivyovaa utachoka mwenyewe. Wakati mwingine hulazimika hata kusimamisha gari na katika mazungumzo ukihoji utaambiwa nasoma chuo fulani.  
Kusimamisha gari msomaji si kwamba ninatamani, la hasha sina maana hiyo bali naepusha mengi likiwemo la kusababisha ajali kwa yale ambayo nayaona yakimulikwa na mwanga angavu wa taa za gari, kwani macho hayana pazia na hayadanganyiki huwezi kufumba macho kuyazuia yasione kilichopo mbele yako. 
Manispaa ya Singida ina jumla ya Vyuo 10 binafsi na vya umma ambapo inakadiriwa kuwepo kwa kundi la vijana wapatao 2300 ambao hutoka mikoa mbalimbali ya Tanzania kuja Singida kwa ajili ya kupata elimu ya taaluma mbalimbali hususani  Ualimu, Utumishi, Uhasibu na ufundi.
 Sioni kama msichana mrembo akivaa mavazi ya heshima urembo wake utapungua bali utazidi kuongezeka.  Tutaiga mavazi  ya aina hii mpaka lini?

No comments: