Friday, October 12, 2012

UTALII NA UVIVU WA WATANZANIA


Na. Matinde  Nestory, Arusha
Leo katika safu hii tutazungumzia utalii wa ndani, ninaposema utalii wa ndani nazungumzia sisi kama watanzania tunatakiwa tujue vivutio vyetu wenyewe mfano kutembelea mbuga zetu, kupanda mlima Kilimanjaro nk.
Ukweli ni kwamba watanzania bado hawajajua umuhimu wa utalii wa ndani hii ni kutokana kwamba wageni wanakuja kutembelea vivutio vyetu lakini sisi wenye vivutio  hatuna hata hamu navyo.
Ni wazi kuwa utalii wa ndani bado haujafikia kiwango cha kueleweka,Tanzania tumebarikiwa kuwa na mbuga kama Tarangire, Serengeti, Ngorongoro, Manyara, Mikumi nk.
Katika mbuga hizo kuna wanyama ambao hawapatikani duniani kote isipokuwa Tanzania, mfano Tarangire kuna tembo wakubwa kuliko mbuga zote. Pia katika mbuga ya Tarangire kuna mibuyu mikubwa ambayo ni vivutio tosha kwa wageni ambao wanakuja na kutalii katika mbuga zetu.
Ninaweza kuthubutu kusema kuwa watanzania bado wako nyuma katika suala zima la utalii wa ndani nini tatizo linalowafanya watanzania kutokuwa na moyo wa kuvitazama vivutio vyao au kuvitembelea labda tatizo ni kiingilio cha kuingia mbugani au tatizo ni kukosa muda wa kuvitembelea, majukumu mengi au ni kuvipuuza vivutio vyao na kusubiri wageni waje na kuvitazama?
Watanzania wanatakiwa kuhamasishwa kuhusu kutembelea vivutio vyao ili waondokane na dhana ya kuwa vivutio hivyo ni vya wageni tu na kujiona wenyewe hawawezi kuvitembelea kwa kutokuelewa kwamba vivutio hivyo ni mali yao wenyewe.
Tumekuwa tukishuhudia wageni kutoka nchi mbalimbali wanakuja na kutaka kupanda mlima Kilimanjaro lakini sisi watanzania hatuna hata hamu ya kutaka  kupanda hata kidogo hata ukifika kituo cha pili katika mlima Kilimanjaro tunajua kwamba mlima Kilimanjaro upo mkoani Kilimanjaro lakini hata wazawa wa mkoa wa Kilimanjaro hawajawahi kupanda wazi ni kwamba watanzania wanatakiwa wahamasishwe kutembelea vivutio vyao.
Mwisho ninawaomba watanzania kwenda kutembelea vivutio vyao na si kusubiri wageni kutoka nje na kuja Tanzania na kujionea vivutio vyetu,pia naiomba serikali ipunguze gharama kwa wananchi wake hii itasaidia watanzania kujifunza mambo mbalimbali,na kuelewa vivutio vyao.

No comments: