Wednesday, November 7, 2012

RAIS KIKWETE AAGIZA UJENZI WA MAABARA


Na. HALIMA JAMAL
SINGIDA  

RAIS wa jamhuri ya muungano wa Tanzania,Dk.Jakaya Mrisho Kikwete,amewaagiza wakuu wa mikoa na wilaya nchini,kujenga maabara mbili za fizikia na kemia kwa kila shule ya sekondari katika kipindi cha miaka miwili kuanzia sasa. Rais Kikwete ametoa agizo hilo juzi wakati akihutubia katika mkutano wa hadhara katika jimbo la Manyoni magharibi mkoani Singida,uliofanyika katika mji mdogo wa Itigi. Alisema maabara ya sayansi ni muhimu mno katika maendeleo ya wanafunzi katika kujifunza kwa nadharia na vitendo. Dk.Kikwete alisema kutokana na umuhimu huo, kunahitajika ushirikiano kama ule ulioonyeshwa wakati wa ujenzi wa shule za sekondari za kata. “Kuhusu uhaba wa walimu,serikali imepanga vizuri na inaendelea kupunguza uhaba huu na lengo ni kuumaliza mapema iwezekanavyo”,alisema. Rais Kikwete ambaye alikuwa kwenye ziara ya siku mbili mkoani hapa ambapo alizindua,kufungua miradi ya barabara na maji,pia aliagiza barabara zinazojengwa kwa gharama kubwa zikiwemo za lami,zilindwe na kutunzwa ili ziweze kudumu kwa muda mrefu.

No comments: