Friday, March 22, 2013

SINGIDA YALIA NA UHABA WA CHAKULA



Na. Boniface Mpagape.

Mkoa wa Singida umeazimia kuweka kipaumbele kwa mazao yanayostahimili ukame ambayo ni mtama, uwele na viazi vitamu ili kuondokana na tatizo la upungufu wa chakula.

Maazimio hayo yamefikiwa katika kikao cha kamati ya ushauri ya mkoa kilichofanyika katika ukumbi wa mikutano wa VETA mkoni humo. Mwenyekiti wa kikao hicho, mkuu wa mkoa wa Singida Dk. Parseko Ole Kone amesisitiza wakulima kulima mazao yanayostahimili ukame, ili kwenda sambamba na hali ya hewa mkoani Singida, kutokana na ukame unaoukabili mkoa huo.

 

Akizungumza katika ufunguzi wa kikao hicho Dk. Kone amesema kwa zaidi ya miaka mitatu mkoa umekuwa na ongezeko la uzalishaji wa mazao ya chakula kutoka tani 442,180 mwaka 2009/2010 hadi tani 575,228 mwaka 2012, sawa na ongezeko la asilimia 30.

 

Amesema uzalishaji wa mazao ya biashara umeongezeka kutoka tani 164,673 mwaka 2009/2010 hadi tani 289,305 mwaka 2011/12 sawa na ongezeko la asilimia 76, na kwamba mafanikio hayo yanatokana na Mkoa kuteua na kufanya juhudi ya kuendeleza mazao ya kipaumbele kwa kuzingatia hali ya hewa. Ameyataja mazao yaliyochaguliwa kwa ajili ya chakula ni mtama, uwele, viazi vitamu na mikunde na mazao ya biashara ni alizeti, pamba, vitunguu na asali.

 

Wajumbe wa kikao hicho kwa kauli moja, wameazimia kuweka msisitizo wa kuzalisha mazao hayo na kwamba uhamasishaji ufanyike ili wakulima washiriki kikamilifu katika kuzalisha mazao hayo.

Aidha, wajumbe wa kikao hicho wamependekeza sheria ndogo ndogo  zitungwe katika kila halmashauri mkoani Singida, ili kuhakikisha kila kaya inakuwa na hekari walau tatu za mazao yanayostahimili ukame, ambayo ndiyo mkobozi kwa wakulima kuondokana na tatizo la uhaba wa chakula. Suala la matumizi mabaya ya chakula pia limejadiliwa katika kikao hicho na wakulima wametakiwa kutumia vizuri chakula wanachokipata.

 

Wajumbe wa kikao hicho pia wamejadili taarifa ya maendeleo ya elimu mkoani Singida, ambapo imeelezwa kuwa matokeo ya kidato cha nne mwaka 2012 mkoa wa Singida ni mabaya. Afisa elimu wa mkoa wa Singida Bi. Fatuma Kilimia amesema mkoa umeweza kufaulisha daraja la kwanza hadi la nne wanafunzi 2272, sawa na asilimia 23.8 kati ya wanafunzi 9,536 waliofanya mitihani hiyo.

 

Kutokana na takwimu hizo, amesema wanafunzi 7264 sawa na asilimia 76.2 walifeli kwa kupata daraja sifuri.

No comments: